Ijumaa , 24th Mar , 2017

Mwamuzi Jacob Adongo aliyechezesha mechi kati ya Simba na Mbeya City iliyofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, amepewa onyo kali kwa kushindwa kutafsiri vizuri sheria za soka.

Mwamuzi Jacob Adongo akizungumza na wachezaji wa timu zote mbili jana

Kadhalika katika mchezo huo Klabu ya Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa timu yake kuingia uwanjani kwa kutumia mlango usio rasmi, hivyo kwenda kinyume na Kanuni ya 14(14) ya Ligi Kuu.

Taarifa iliyotolewa leo na TFF, imesema pia klabu ya Yanga imepewa onyo kali kutokana na benchi lake la ufundi kumlalamikia mara kwa mara Mwamuzi wakati wa mechi ya utangulizi ya U20 kati ya timu hiyo na Simba iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 

Taarifa hiyo ambayo haijaeleza kamati iliyohusika na adhabu hizo, imesema kuwa katika mechi namba 190 (Kagera Sugar 1 vs Majimaji 0), Klabu ya Majimaji imepigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) kwa kosa la kutokuwa na Daktari kwenye Kikao cha Maandalizi ya Mechi (Pre Match Meeting) na hata uwanjani wakati wa mchezo. 

Pia kwa kutumia Kanuni ya 9(8) ya Ligi Kuu imefuta kadi ya njano aliyooneshwa mshambuliaji Jaffari Salum wa Mtibwa Sugar katika mechi hiyo namba 175 kati ya African Lyon na Mtibwa Sugar iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam baada ya kubaini haikuwa sahihi.

Katika Ligi daraja la Pili, mechi namba 3 (Oljoro 1 vs Transit Camp 1). Klabu ya Oljoro imepigwa faini ya sh. 200,000 (laki mbili) kutokana na washabiki wa timu hiyo kumrushia mawe Mwamuzi akiwa uwanjani.