Alhamisi , 12th Jan , 2017

Michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara inataraji kuendelea mwishoni mwa wiki kuanzia kesho ambapo JKT Ruvu na Ruvu Shooting zinatarajiwa kuchuana kesho Ijumaa Januari 13, 2017 kwenye Uwanja wa Mabatini, ulioko Mlandizi mkoani Pwani.

Mechi ya ligi ligi kuu kati ya Mbeya City na Azam

Mbali ya ‘derby’ ya JKT Ruvu na Ruvu Shooting, Jumamosi Januari 14, 2017 kutakuwa na mchezo mwingine wa upinzani kati ya Stand United na Mwadui FC – zote za Shinyanga na zitapambana kwenye Uwanja wa CCM Kambarage.

Kadhalika siku hiyo ya Jumamosi Januari 14, 2017 Kagera Sugar itakuwa mwenyeji wa Ndanda FC ya Mtwara kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba katika mchezo mwingine wa VPL.

Jumapili Januari 15, 2017 kutakuwa na mchezo mmoja tu wa Ligi Kuu ya Vodacom ambako Mbao itakuwa mwenyeji wa African Lyon ya Mwanza katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Kadhalika Jumatatu Januari 16, 2017 kutakuwa na mchezo mmoja tu ambako Tanzania Prisons itakuwa mgeni wa Toto Africans kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Michezo mitatu ambayo haikupangiwa tarehe hapo awali kwa alama ya TBA ikiwa na maana ya kutajwa baadaye (To Be Announced), tayari Bodi ya Ligi imepanga tarehe.

Tarehe hizo ni Januari 17, 2017 – siku ya Jumanne kutakuwa na mchezo mmoja kati ya Majimaji itakayowaalika mabingwa watetezi wa taji la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Young Africans ya Dar es Salaam katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Majimaji mjini Songea mkoani Ruvuma.

Kadhalika mechi nyingine ziliopangiwa tarehe na muda ni kati ya Mtibwa Sugar itakayocheza na Simba, Jumatano Januari 18, 2017 kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro wakati Azam itakuwa mwenyeji wa Mbeya City kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Mbagala jijini Dar es Salaam.

Mchezo huu wa Azam na Mbeya City utaanza saa 1.00 usiku wakati michezo yote tajwa hapo juu itaanza saa 10.00 jioni