Jumatatu , 11th Sep , 2017

Msemaji wa Klabu ya Simba Haji Manara amerusha jiwe gizani na kudai klabu ya Simba ni klabu ya watu ndiyo maana inatajwa kama taasisi maarufu na kudai mtu anayepingana na hilo akapambane na kuwalipa mshahara wachezaji wake.

Msemaji wa Klabu ya Simba Haji Manara

Kupitia ukurasa wake wa Instagram Manara ameweka ujumbe huo hali ambayo imezua majadiliano huku mashabiki wa Simba na Yanga wakirushiana maneno kutokana na kuwa na upinzani mkubwa kwenye Soka la Tanzania.

"Simba ni klabu ya watu(Peoples Club) watu wa jinsia zote,dini zote, makabila na rangi zote, vyama vyote, ndiyo maana kwa sasa inatajwa kuwa taasisi maarufu kupita zote nchini, ukibisha kapambane na kulipa mishahara wachezaji wako" alisema Manara. 

Aidha mashabiki wa soka wengi wamedai kauli ya Manara imekuja baada ya mchezaji wa Yanga ambaye alitokea Simba Ibrahim Ajib kuanza kuonyesha makali yake kwenye mchezo wao wa jana na Njombe Mji  kwa kutupia bao 1 huku Simba wakishindwa kuambulia kitu kwenye nyavu za Azam FC katika mchezo wao uliochezwa Jumamosi Septemba 9, 2017.