Jumanne , 10th Jan , 2017

Kocha mkuu mpya wa Azam FC ambaye ametambulishwa leo, Mromania Aristica Cioaba ameingia kwa mkwara mzito na kusema kuwa anaijua vizuri klabu ya Azam na analijua vizuri soka la Afrika huku akielezea furaha yake baada ya kupata kibarua hicho hicho.

Aristica Cioaba, Kocha mpya wa Azam

 

 Cioaba amesema kuwa anafuraha kubwa leo hii kusaini mkataba wa kuifundisha timu hiyo huku akiahidi kazi nzuri na kuifanya timu hiyo kuwa bora barani Afrika.

“Najua Azam FC hapa Tanzania ni moja ya timu kubwa yenye historia huko nyuma, napenda kuushukuru uongozi kwa kuniamini na kunipa nafasi kuja kufundisha soka kwenye nchi hii, kwa mashabiki napenda kuwaambia kuwa nalijua soka la Afrika, nimewahi kufundisha Ghana na kupata matokeo mazuri.

“Kuhusu wakati ujao, nina furaha sana kuhusu uongozi walipoongea na mimi wakati tunaweka mipango ya timu ya hapo baadaye na hili ni jambo zuri kwa kocha, kitaaluma nawaahidi mashabiki na watu wote wanaoipenda Azam FC, niko hapa kuwapa mambo mazuri katika kazi yangu kwenye klabu,” alisema.

Msimu uliopita, Cioaba aliiongoza Aduana Stars ya Ghana kushika nafasi ya pili kwenye Ligi Kuu ya Ghana, ambapo anafahamiana kwa ukaribu na nyota wawili wa Azam FC, Yakubu Mohammed na Yahaya Mohammed, waliosajiliwa kutoka timu hiyo katika usajili wa dirisha dogo.

Mbali na kufundisha soka nchini Ghana pia amewahi kufanya kazi kwenye miamba ya Morocco, Raja Casablanca, Al Masry ya Misri na katika nchi za Romania, Kuwait, Oman na Jordan.