Jumapili , 22nd Oct , 2017

Dereva wa Mercedes Lewis Hamilton huenda leo akaibuka bingwa wa mbio za magari duniani Formula1 endapo atashinda kwa pointi nyingi kwenye mbio za leo nchini Marekani (USGP).

Hata hivyo Hamilton ana nafasi ya kufanya hivyo baada ya kujihakikishia nafasi ya kwanza kwenye mpangilio wa magari wakati wa mbio hizo. Mkali huyo wa gia kutoka nchini Uingereza ameongoza mbio za kusaka nafasi kwenye kupanga magari ambapo sasa leo ataanza wa kwanza.

Mpinzani wake wa karibu Sebastian Vettel kutoka timu ya Ferrari amemaliza wa pili hivyo gari yake itasimama kwenye nafasi ya pili wakati wa mbio za USGP leo akifuatiwa na gari ya Valtteri Bottas wa Mercedes ambaye atakuwa wa tatu.

Mbio zitafanyika jioni ya leo kwenye mitaa ya Austin jijini Texas Marekani. Hadi sasa Lewis Hamilton anaongoza mbio hizo akiwa na alama 306 mbele ya Sebastian Vettel mwenye pointi 247.

Baada ya mbio za leo za USGP zitakuwa zimebaki mbio 3 ili kumaliza msimu wa 2017 ambazo ni Mexico Grand Prix, Brazilian Grand Prix na Abu Dhabi Grand Prix.