Jumatano , 3rd Jun , 2020

Msanii Natasha Lisimo ambaye zamani alikuwa anafahamika kwa jina la Khadja Nito amesema, alipitia magumu alipoenda kwa mganga na kuambiwa kutekeleza maagizo kwa kupewa hirizi, kuchinja Kuku, Mbuzi na kulala makaburini pamoja na kutupiwa ugonjwa wa UKIMWI.

Msanii wa injili Natasha Lisimo

Akizungumza kwenye kipindi cha MamaMia ya East Africa Radio, kinachoruka kila siku ya Jumatatu hadi Ijumaa kuanzia 4:00 Asubuhi hadi 6:00 mchana, Natasha Lisimo amesema licha ya kwenda kwa mganga lakini bado aliona mambo yake yanamuendea vibaya.

"Utaenda kwa mganga kama mambo yako hayakai sawa au watu kupoteza interest na wewe, mimi nilivyoenda kwa mganga hakukuwa na matokeo mazuri bali niliona giza zaidi, Mganga aliniambia nimepandikiziwa ugonjwa wa ukimwi nikamwambia akome kwamba sina ugonjwa huo, nia yangu nilivyoenda kwa mganga nilitaka mambo yangu yaonekane nipate kazi au show" ameeleza Natasha Lisimo.

"Nimeshachinja Kuku, Mbuzi na kulala makaburini, waganga waongo sana wanakwambia mtu fulani au msanii anakuibia nyota yako na anakutajia hadi jina kabisa, kuna siku akamhusisha Mama yangu mzazi nili-mind na kuanza kumkaripia hapohapo nikaondoka" ameongeza.

Kwa sasa msanii huyo ameokoka na ameachana na miziki ya kidunia na anaimba nyimbo za Injili.