Jumanne , 26th Sep , 2017

Mbunifu wa mavazi maarufu hapa bongo Martin Kadinda ambaye pia ni meneja wa msanii Wema Sepetu, amesema anapata wakati mgumu kumsimamia msanii huyo mkubwa na mrembo, kutokana na tabia zake zisizobadilika, ikiwemo kutokuwa kimawazo.

Martin Kadinda ameyasema hayo alipokuwa akipiga stori na Big Chawa kwenye Planet Bongo ya East Africa Radio, na kusema kwamba licha ya Wema Sepetu kuwa mtu muhimu kwenye maisha na kazi zake, amekuwa mtu ambaye habadiliki, hivyo inamuwia vigumu kumtengenezea mazingira mazuri ya kazi zake na kesho yake.

'Changamoto kubwa kwake unajua Wema ni mtoto hakui, yani miaka inakwenda bado yuko vile vile, kikubwa ni kuweza kumtengenezea mazingira ili kesho na kesho kutwa aweze kuheshimika”, amesema Martin Kadinda.

Martin ameendelea kwa kusema kwamba ...”Wema ana maisha yake binafsi, ana vitu vyake anavyovipenda kwa hiyo ninachokifanya zaidi ni kuweza dhibiti mambo yake binafsi yasimfanye kesho na kesho kutwa kushindwa kupata ugali wake wa kila siku”.

Kwa sasa Martin Kadinda amesimama kumsimamia msanii huyo kutokana na kubanwa na masomo, huku akisema kwake atabaki kuwa msimamizi wa msanii huyo pale panapohitajika mchango wake.