Jumanne , 10th Jan , 2017

Msanii wa muziki wa taarab nchini ambaye hivi sasa anatesa na kundi la Wakali wao, Khadija Yusuf amesema hajawahi kuzungumza kitu chochote na wifi yake ambaye pia ni mwimbaji wa taarab, Leila Rashid kwa kipindi cha zaidi ya miaka minne.

Khadija (kushoto) akiwa na kaka yake Mzee Yusuph

 

Khadija ametoa nyeti hiyo alipokuwa kwenye kipindi cha FNL cha EATV, alipokuwa akifafanua kuhusu madongo anayotupiana na wifi yake huyo, ambapo ilikuwa ikidaiwa kuwa Khadija aliimba wimbo unaomlenga Leila ukimtaarifu kuwa talaka yake iko njiani.

"Sijaongea na Leila miaka mitano, mara ya mwisho nilimsalimia salam Aleykum, lakini hakuitikia, basi, tangu hapo sijaongea naye tena" Alisema Khadija huku akisisiza kuwa hana ugomvi wowote na Leila na kwamba wimbo aliouimba haukumlenga yeye.

Leila ni mke wa Mzee Yusuph kaka wa Khadija Yusuph na tangu Mzee alipotangaza kuacha muziki, pamekuwa na vita ya maneno kati ya mawifi hao, Leila na Khadija, huku kukishuhudiwa kundi la Jahazi Modern Taarab likisambaratika kwa kasi ya aina yake.