Alhamisi , 27th Jul , 2017

Msanii Baraka The Prince amefunguka kwa kudai sababu kubwa zilizomfanya yeye kujiengua katika usimamizi wa kampuni ya RockStar4000 ni kutokuwa makini na ukweli katika kazi wanazozifanya dhidi yake.

Msanii Baraka.

Baraka amebainisha hayo kupitia kipindi cha eNewz kutoka EATV baada ya kuona takwimu zake zimezidi kushuka katika kazi zake alizokuwa anasimamiwa na uongozi huu pamoja na kutolewa nyimbo moja kwa mwaka tofauti na yeye alivyokuwa anategemea atafanya.

"Nimeamua kufanya hivyo kwa sababu hii ndiyo kazi yangu na mwisho wa siku hii mimi ndiyo kila kitu na sina kazi nyingine, kwa hiyo nikiona kuna vitu havipo 'serious' na havipo 'sure' kwa upande wa watu ninaofanya nao kazi sina budi kujiengua na kufanya mwenyewe. Nipo sawa na hakuna mtu ambaye anaweza kuniingilia juu ya hilo mwisho wa siku mimi ndiyo ninajua kazi ninayofanya na ugumu wake katika kujenga 'brand' yangu, najua ugumu wa kila kitu 'so' haya ni maamuzi yangu", amesema Baraka.

Pamoja na hayo, Baraka ameendelea kwa kusema "mimi ndiyo mwenye kauli ya mwisho. Sitaki kuongelea masuala ya mikataba kwa sababu kipindi nina saini tokea awali sikuweza izungumzia wakati naingia kwa hiyo sitasema lolote juu ya hilo kwa sasa",amesisitiza Baraka.

Kwa upande mwingine, Baraka amesema yeye hafanyi muziki kwa ajili ya menejementi bali anafanya muziki kwa mashabiki wanamuwezesha kumlipa katika nyimbo zake wanazozipakua katika mitandao.