Jumatano , 23rd Aug , 2017

Msanii wa muziki wa kizazi kipya Mr. Blue ametoa siri inayomfanya afanikiwe kufanya vizuri kwenye 'game' ya bongo fleva tangu aanze akiwa mdogo na kusema kuwa haikuwa rahisi kwake wakati anaanza kwani wengi walimtupia maneno yenye madongo ndani yake.

Akizungumza na mwandishi wa East Africa Radio, Mr. Blue amesema kipindi anaanza kutengeneza 'brand' yake kama bishoo watu wengi walimbeza kwa kumtolea maneno asiyostahili mpaka kupelekea kukosa msaada kwa wenzake, wakiamini kuwa ametokea katika familia ya kitajiri, kumbe haikuwa hivyo.

“Niliona hamna rapper ambaye alijitokeza kama style fulani ya kibishoo, kwa hiyo nikabuni style yangu japokuwa sikuwa bishoo, namshukuru Mungu mara ya kwanza nilipigwa sana mawe, watu waliniona kama huyu dogo kwao kuna hela nikakosam misaada”, alisema Mr. Blue.

Hata hivyo katika siku za hivi karibuni, msanii Dully Sykes alimtaja Mr. Blue kuwa ni miongoni mwa wasanii wachache waliyofanikiwa katika kujiwekea misingi mizuri ya kazi zake na  hata asipoachia kazi kwa muda mrefu watu wataendelea kukubali uwepo wake kwenye 'game'.

Msikilize hapa chini Mr. Blue, akielezea jinsi alivyokuwa anabaniwa kwa kuaminika ana uwezo kifedha.