Jumatano , 18th Jan , 2017

Msanii wa bongo fleva Ditto amesema anajipanga kurudi na mfumo wa  kuachia albam ya nyimbo zake mwishoni mwa mwaka huu japo haijazoeleka kwa wasanii wa Tanzania.

Ditto

Uamuzi huo wa kutoa albam unamfanya awe ameungana na wazo la kundi la muziki huo la Navy Kenzo ambao pia mwishoni mwa mwaka jana walitangaza kuja na albam ya ngoma zao inayokwenda kwa jina la AIM hivyo inawezakana Ditto akawa ametekwa kimawazo na 'idea' hiyo ya albam kutoka kwa Navy Kenzo.

Akiongea kupitia eNewz Ditto amesema kwa sasa anaendelea kurekodi nyimbo nyingi ili hapo baadaye aweze kuchagua ni zipi ambazo zinafaa kukaa kwenye albam yake ingawa kwa sasa ataachia nyimbo mbalimbali ili kuweza kurudisha mashabiki zake na kurudisha hadhi yake ya zamani.

Pia Ditto amesema kwa sasa anajipanga kutengeneza utamaduni wake na akifanikiwa kwa hilo atajiingiza kwenye biashara za kuachia albam mbalimbali na pia amewashukuru mashabiki kwa kuupokea vyema wimbo wake wa moyo sukuma damu.