Ijumaa , 21st Apr , 2017

Msanii wa muziki wa bongo fleva Lulu Diva amefunguka na kusema kuwa marafiki wa kike si watu wazuri kwani ni watu ambao wanaweza kukufanyia mambo mabaya na kukuumiza zaidi kwa mambo yako.

Lulu Diva

Lulu Diva alisema haya alipokuwa akiongea na EATV na kusema yeye saizi hawaamini kabisa marafiki wa kike kutokana na ukweli kwamba rafiki yake wa karibu alitembea na mchumba wake jambo ambalo lilimuumiza sana.

"Mimi sina marafiki wa kike na wala siwaamini kabisa, sababu nilikuwa na rafiki ambaye nilikuwa nashauriana naye na kumuweka wazi kila kitu changu na yeye aliniweka wazi kwa kila kitu, alikuwa ananipenda sana kiasi kwamba sikuwahi kufikiria kama angeweza kutembea na mchumba wangu, lakini huwezi kuamini niliwafuma na mchumba wangu chumbani kwangu na kiukweli niliumia sana kwa kuwa yule mwanaume nilikuwa nampenda sana" alisema Lulu Diva 

Mbali na hilo Lulu Diva anasema kitendo hicho alichofanya huyo mchumba wake kilimfanya kuwatambua wanaume kuwa wakipendwa ni tatizo, wakioneshwa mapenzi wanakuwa na matatizo zaidi. Hivyo Lulu Diva anasema anashukuru Mungu hayo mambo yalipita lakini yamemjenga sana na kumfunza pia.