Jumamosi , 19th Aug , 2017

Muigizaji mkongwe nchini Jacob Stephen 'JB amefunguka na kudai wamepata mkombozi katika usambazaji wa kazi zao za filamu huku akiwataka mashabiki zake kukaa mkao wa kula wa kupokea kazi mpya kutoka kwake baada ya kukaa kimya kipindi kirefu.

Muigizaji mkongwe nchini Jacob Stephen 'JB.

JB amebainisha hayo wakati akizungumza na mashabiki zake kupitia ukurasa wake wa 'Instagram Live' na kusema baada ya kupitia changamoto nyingi katika suala zima la usambazaji, sasa hivi wamepata kampuni mpya ambayo itakuwa inauza kazi za wasanii kwa kutumia simu za mikononi.

"Ukiachilia mbali matatizo ya ubora wa picha, hadhithi na uigizaji wa filamu zetu za kibongo, tatizo lingine kubwa linalotukabili tasnia ya filamu ni usambazaji ambapo kwa kipindi kirefu watayarishaji wa filamu wamekuwa wakikumbana nalo lakini sasa tumepata suluhisho ya tatizo hilo", alisema JB.

Pamoja na hayo, JB aliendelea kwa kusema "tumepata Kampuni mpya ya usambazaji ambapo sasa hivi mashabiki zetu sasa wataweza kununua filamu zote ziwe za zamani au mpya kwa kutumia simu zao za mkononi kama wanavyofanya wakitaka kununua umeme Tanesco, kwa kuweka namba husika ya filamu anayohitaji na baada ya hapo atapelekewa hicho alichonunua mpaka nyumbani kwake kwa kutokana namna aliyojaza katika maelezo yake aliyoyafanya kabla ya kununua".

Kwa upande mwingine, JB amesema hapo awali walikuwa wakikumbana na changamoto nyingi katika usambazaji wa kazi zao kwa kuwa alikuwa ni mmoja mkubwa, ambaye ikafikia hatua hawezi kupokea filamu zilizo gharimu kiasi kikubwa kwa kuogopa hasara.