Jumamosi , 23rd Sep , 2017

Msanii Young Dee amesema kitendo cha msanii mwenzake Dogo Janja kumtolea maneno machafu na kumtuhumu kuendelea kutumia madawa ya kulevya, ni kumvunjia heshima kwani yeye ana mchango mkubwa kwenye maisha yake, na pia inaonyesha hana akili.

Akizungumza na mwandishi wa East Africa Television, Young Dee amesema kama asingekuwepo yeye hata Dogo Janja asingekuwepo, na inadhihirisha ni jinsi gani bado hajakua kiakili.

"Yeye kama anaongea kuhusu suala la madawa inabidi awe na ushahidi, kwa sababu mimi nimeongea niko na ushahidi kwamba kimuziki asingekuwepo Young Dee wala wao wasingekuwepo, mimi nina mchango kwenye muziki wao, aliposikia mimi naongea vile ilibidi ajiulize kwa nini nimekasirika, sasa kuanza kurusha maneno inaonyesha ni upumbavu na hana akili, inaonyesha ni jinsi gani bado mtoto", amesema Young Dee.

Pamoja na hayo Young Dee ameendelea kwa kusema kwamba ikibidi atamshikisha adabu msanii huyo, kwani sio mara ya kwanza amekuwa akimuimba na kumrushia maneno yenye chokochoko. 

"Unajua unakuwa mstaarabu sana lakini kuna muda unashindwa, mimi sijawahi kumuimba mtu, lakini hawa machalii wamekuwa wakiniimba kila siku sasa inabidi ifike mwisho", amesema Young Dee.

Hivi kaibuni kumeibuka mgogoro mkubwa kati ya wasanii watatu akiwemo Young Killer, baada ya Young Dee kutaka kutofananishwa nao, na Dogo Janja kujibu kwamba Young dee anatumia madawa ya kulevya hivyo ni mtu ambaye hatakiwi kutiliwa maanani.