Ijumaa , 23rd Jun , 2017

Msanii Ben Pol amefunguka ya moyoni baada ya kukutana kwa mara ya kwanza na mchekeshaji Ebitoke kwa kusema anaamini watu wengi wameoa ama kuolewa na watu wasiowapenda kwa sababu ya kushindwa kuelezea hisia zao.

Ben amebainisha hayo kupitia ukurasa wake wa instagram baada ya mchekeshaji Ebitoke kuonesha hisia za mapenzi katika mitandao ya kijamii kwa takribani majuma mawili hivi sasa.

"Hakuna kitu kizuri kama kujishusha na kukubali kujifunza pale unapoona kuna jambo zuri la kujifunza, ikiwa unampenda mtu au unatamani nafasi fulani, utajuaje kama unaweza kuipata hiyo nafasi au la ikiwa haujaiomba kwa muhusika ?. Naamini watu wengi sana wameoa ama kuolewa na watu wasiowapenda kwa sababu tu walipoteza nafasi za kuwaambia hisia zao wale wawapendao. Mwishowe walipokuwa tayari kuwaambia ikawa 'too late" aliandika Ben Pol.

Pamoja na hayo, Ben aliendelea kusema "Ikumbukwe humu duniani sisi sote tunapita na labda huyo mtu kesho hatokuwepo. Ebitoke umenifundisha jambo kubwa sana maishani, najua wengi walikubeza sana wengine walikuambia hautaweza hata kuonana na mimi laini huwezi amini mimi nimefurahi mno, kukutana na wewe na kuongea" alisisiza Ben Pol

Kwa upande mwingine Ben amesema amepata jambo kubwa sana kupitia Ebitoke na kuahidi kuyaishi maneno yake siku zote mwa maisha yake.