Jumatatu , 13th Nov , 2017

Serikali imekiri kujitoa kwenye Mpango wa Kimataifa wa uendeshaji wa shughuli za serikali kwa uwazi (OGP), ambao serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilijiunga Septemba 21 mwaka 2011.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Mh. George Mkuchika wakati akijibu swali la Mbunge wa Kigoma Mjini Mh. Zitto Kabwe lililohoji kwanini serikali imejitoa kwenye Mpango wa Kimataifa wa uendeshaji serikali kwa uwazi (OGP).

Mh. Mkuchika amesema baada ya serikali kushiriki kwenye utekelezaji wa mpango huo kwa muda wa miaka minne imeamua kujitoa, ambapo ameongeza kuwa sio nchi ya kwanza kujitoa kwenye mpango huo.

“Baada ya serikali kushiriki utekelezaji wa mpango huo kwa muda wa miaka minne imeamua kujitoa, na Tanzania sio nchi pekee iliyojitoa, zipo nchi kama Hungury na Urusi zilijiunga na baadae kujitoa”, amesema Waziri Mkuchika.

Kwa upande mwingine Mh. Zitto ameshauri kuwa serikali ingeendelea kuwa mwanachama wa (OGP) ingefaidika kwa sulaa la ndege za Bombadier ambazo zimekwama nchini Canada kutoka na nchi huyo kuwa ndiyo mwenyekiti wa sasa wa OGP.

Hata hivyo Waziri amesisitiza kuwa mahusiano ya Tanzania na Canada ni mazuri bila hata ya Tanzania kuwa mwananchama wa (OGP) ambapo masuala ya Bombadier yatashughulikuwa na balozi wa Tanzania nchini humo.

Mpango wa kuendesha serikali kwa uwazi ulizinduliwa Septemba 20 mwaka 2011 na rais wa zamani wa Marekani Barack Obama ikiwa kama taasisi binafsi. Hadi sasa umoja huo una nchi wanachama 70 ambapo nchi 10 pekee ndio zinatoka barani Afrika.