Jumatano , 22nd Nov , 2017

Waziri  wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt Mwigulu Nchemba amewakosoa upinzani kutumia tukio la kushambuliwa kwa risasi Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu kama ajenda katika kampeni za uchaguzi wa marudio na kusema kwamba chama hicho kimefilisika.

Akiwa Masasi katika kampeni za kumnadi mgombea wa udiwani wa tiketi ya CCM, Dkt Nchemba amesema kwamba kitendo hicho cha Chadema kufanya kila mahali tukio la Lissu kama ndiyo ajenda atakwenda kuwaambia wakazi wa Singida wawaangalie vizuri watu hao.

"Mimi nitaenda kuwaambia wana Singida kwamba tuwaangalie vizuri hawa watu. Wao  ni mwenzao kwenye Chama sisi ni ndugu yetu na tunatoka sehemu moja. Inawezekanaje wawe wanafurahia tukio hilo? Kama kuna kitu walikuwa wanataka kitokee ili warushe maneno kwa serikali" amesema Dkt Nchemba.

Aidha akiendelea Nchemba amesema Chadema wanamuona kama Lissu mtaji ndiyo maana hata polisi walipomtaka dereva wake ili kuweza kumhoji wameamua kukaa naye huko.

Pamoja na hayo Nchemba amewata watu wakapige kura bila kuhofia fujo zinazoweza kufanywa na wanachadema kwani serikali ipo kwa ajili ya kusimamia sheria.

 "Wamezoea kufanya fujo. Nendeni mkapige kura akitokea mtu atakayethubutu kukughasi wewe mkariri sura alafu sisi tutamfundisha ustaarabu wa vyama vingi. Anayefanya fujo atakutana na mkono wa sheria. Na uzuri vijana wangu wapo hapa atakayethubutu kufanya fujo, Muwaonyeshe kwamba mmepitia mafunzo" Nchemba

Hata hivyo Nchemba amewataka wananchi hao kuichagua CCM kwa kazi nzuri inayofanya na kuwaamba kuuchagua upinzani wakitegemea itashinda ni sawa na kujeruhi nafsi.