Alhamisi , 26th Nov , 2020

WAFANYABIASHARA wawili wamefikishwa mbele ya Mahakamaya Hakimu Mkazi Kisutu Jijini Dar es salaam wakikabiliwa na makosa matano ikiwemo la utakatishaji fedha kiasi cha shilingi za kitanzania zaidi ya milioni 11.

Pichani: Mfano wa mikono ya mtu iliyofungwa pingu

Moses Michael (35) mkazi wa Mwanza na Felix Nyangai (38) mkazi wa kibamba CCM wamesomewa mashtaka hayo mbele ya  Hakimu Mkazi Mkuu Rashid Chaungu na wakili wa serikali mwandamizi Wankyo Simon ambapo amedai kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika na kesi hiyo itatajwa tena Desemba 3 mwaka huu.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka inadaiwa kati ya Septemba 3, 2020 na Novemba 7, 2020 katika Maeneo yasiyojulikana huko Mwanza na Dar-es-Salaam washtakiwa hao waliongoza genge la ualifu na kujipatia Sh. Milioni 11,210,000.

Shtaka la pili, inadaiwa  Septemba 5, 2020 eneo la Mlimani city, washtakiwa walijipatia Pesa kwa njia ya udanganyifu kiasi cha Sh. Mil 9,600,000 kwa nia ya kuonesha kwamba pesa ni kwa ajili ya malipo ya leseni na kibali kwa ajili ya kusafirisha madini aina ya dhahabu kutoka CRDB kwenye akaunti namba 01522406097400 yenye jina la  Moses Michael kutoka kwa Jonathan Mkasa.

Shtaka la tatu, Septemba 10, 2020 eneo la Mlimani city jijini Dar-es-Salaam,  CRDB kwenye akaunti namba 01522406097400 yenye jina la Moses Michael, washtakiwa walijipatia pesa kwa njia ya udanganyifu Sh.Mil 1,160,000 kwa ajili ya kibali cha kusafirisha madini huku wakijua kuwa ni uongo.

Inadaiwa, Septemba 11, 2020 eneo la Mlimani city washtakiwa walijipatia pesa kwa njia ya udanganyifu CRDB Kiasi cha Sh. Laki 450,000 kwenye akaunti namba 01522406097400 yenye jina la Moses Michael kutoka kwa Jonathan Mkasa kwa lengo la malipo ya leseni na kibali cha kusafirisha madini aina ya dhahabu huku wakijua kuwa siyo kweli.

Katika shtaka la mwisho inadaiwa kati ya Septemba 3,2020 na Novemba 7,2020  katika maeneo tofauti ya Mwanza na Dar-es-Salaam, washtakiwa walitakatisha pesa alamu kutoka CRDB kiasi cha Sh.Mil 11,210,000 kwenye akaunti namba 01522406097400 yenye jina la Moses Michael kutoka kwa Jonathan Mkasa kwa lengo la malipo ya leseni na kibali cha kusafirisha madini aina ya dhahabu huku wakijua kuwa siyo kweli.