Alhamisi , 25th Aug , 2016

Watanzania nchini Wametakiwa kuwekeza na kujikwamua kiuchumi kwa kuanzisha viwanda vidogovidogo vitakavyozalisha ajira na kukuza pato la nchi hivyo kusaidia kuondokana na tatizo la umasikini uliokithiri kwenye kaya nyingi nchini.

Afisa Tarafa wa Kimandoru mjini Arusha, Felician Mtahengerwa.

Hayo yamebainika kutoka kwa Washiriki wa Mafunzo ya Ujasiriamali juu ya namna ya kumiliki viwanda vidogo vya uzalishaji, yalioandaliwa na Kampuni ya Zebra iliyoko jijini Arusha kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali hao kukuza mitaji yao.

Suzan Nyari na Glory Antony wamesema kuwa Mafunzo waliyoyapata juu ya jinsi ya kutengeneza bidhaa za viwandani kama Sabuni, Ufugaji wa kuku pamoja na usindikaji vyakula yatawasaidia katika kuanzisha viwanda vidogovidogo hivyo wameiomba serikali iwapatie mikopo ya riba nafuu ili kutekeleza adhma ya Rais Magufuli ya kuwa na uchumi wa viwanda.

Naye Mkurugenzi wa kampuni iliyotoa mafunzo hayo, Zuberi Mwinyi amesema kuwa Mafunzo wanayoyatoa yatawasaidia wananchi wa jiji la Arusha kuweza kutumia vizuri fursa zilizopo katika maeneo yao kujikomboa kiuchumi.

Kwa upande wa Afisa Tarafa wa Kimandoru mjini Arusha Felician Mtahengerwa amesema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia Wananchi wa Arusha kufanya biashara kitaalam na kwa kuzingatia sheria na maadili ili waweze kuepuka hasara.