Jumatatu , 5th Dec , 2022

Waumini wa kanisa la EAGT jimbo la Mwanza kusini wamekumbwa na taharuki baada ya kukuta kanisa lao limebadilishwa jina bila wao kujua hali iliyozua mzozo katika kanisa hilo na kusababisha shughuli zote za ibada kukwama

Wakizungumza na EATV viongozi wa kanisa hilo wamesema mgogoro huo uliibuka siku nne zilizopita lakini ghafla wakashangaa Jumapili wakakuta jina la kanisa hilo limebadilishwa na kuandikwa ASSEMBLIES OF GOD GOSPEL CHURCH INTERNATIONAL AGGCI na wakishindwa kuelewa nini kimetokea huku umiliki wa eneo hilo ukisoma kwa jina la kanisa la EAGT

Mchungaji Boaz Kazeba ndiye anadaiwa kubadilisha kanisa hilo la EAGT na kuwa AGGCI lililopo eneo la Bugarika mtaa wa Zahanati kata ya Pamba jijini Mwanza

"Sikutaka nifanye kitu chochote kile lakini umesikia wameniita mimi gaidi sijui muhuni, elishababu sijui nashangaa na huyo aliyesema mimi ni muumini wangu wa zamani anayosema ametoa kiwanja ana vielelezo? Hapa sisi tulimjengea mtu nyumba ya vyumba vitatu na maandishi ninayo siyo kama nazungumza kitu ambacho hakipo" ameeleza mchungaji Boaz

Mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Zahanati Mashaka Nkonyoka amesema bado kanisa hilo lipo chini ya umiliki wa EAGT

"Lakini kimsingi kanisa hilo linaendeshwa na EAGT kama waanzilishi wa kanisa hilo siku zote ipo hivyo sasa imetokea kama wiki moja iliyopita mchungaji wa kanisa hilo Boazi Kazeba kubadilisha jina la kanisa hilo kutoka EAGT  na kuwa AGGCIA yani kanisa jipya"

Hadi EATV inatoka katika eneo hilo bado kanisa hilo lilikuwa limefungwa huku viongozi wa pande zote mbili wakipelekwa polisi kwa ajili ya mahojiano ili kutafuta suluhu ya mgogoro huo