Jumanne , 21st Feb , 2017

Wasanii wa nyimbo za Singeli wamelalamikiwa kwa kukosa ubunifu katika kazi zao ndiyo maana mpaka sasa hakuna mtu yeyote aliyeweza kuachia 'ngoma' mpya kwa kuwa wote wanategeana.

Msaga Sumu

Kilio hicho kimetolewa na Msaga Sumu ambaye ndiye aliyekuwa msanii wa kwanza kuutambulisha muziki huo kutoka uswahilini kwa kurekodi na kuruhusu kazi zake kuchezwa katika vituo mbalimbali vya Radio na Television, kiasi cha kujipa jina la Mfalme wa Singeli

"Singeli imekuja baada ya mimi kuanzisha muziki wa radha, kuna siku niliongea itafikia wakati singeli itapotea kwasababu wasanii wengi kuwa wavivu wa kufikiri pamoja na ubunifu wa kutengeneza kazi zao wenyewe lakini wao wanachokifanya ni kunisubiri Msaga Sumu nitoe wimbo kisha waende kugeuza maneno". Alisema Mfalme huyo

Aidha Msaga Msumu ambaye amezungumza kupitia eNewz ya EATV amesema soko la muziki huo limeshuka kwani hapo awali lilikuwa limepanda juu na kufanya vizuri zaidi lakini sasa hivi wameshuka chini zaidi. 

Vilevile msanii huyo amesema baadhi ya wanasingeli hawana ushirikiano kwa kujiona wameshafika katika hatua kubwa za maendeleo kwa kutoa kazi moja tu.

Msanii huyo aliendelea kwa kusema kwamba wakitaka muziki wa singeli usimame lazima washirikiane na wasitake kuvimba kwa kutoa ngoma mbili pia amewataka wasanii wenzake kutokata tamaa kwani bado nafasi wanayo kwakuwa muziki wa bongo fleva haujawaacha mbali sana.