Ijumaa , 24th Mar , 2017

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amepiga marufuku shule za binafsi na serikali kupokea wanafunzi bila kupimwa ugonjwa wa Kifua Kikuu (TB)

Ummy Mwalimu

Pia Waziri Ummy ameagiza watu walio katika makundi hatarishi wakiwemo wanaoishi na maambukizi ya UKIMWI na wajawazito wafike vituo vya Afya kupimwa Kifua Kikuu (TB).

"Ni marufuku kwa Shule za bweni za umma na binafsi pamoja na vyuo kupokea mwanafunzi ambaye hana uthibitisho wa kuchunguzwa ugonjwa wa TB. Hatutamvumilia Daktari/Mganga atakae-sign na kutoa Cheti cha Uchunguzi wa Magonjwa ukiwemo Ugonjwa wa TB kwa Mtu ambae hajafanyiwa Uchunguzi". Amesema Ummy

Akitoa maagizo hayo leo Jijini Arusha kwenye maadhimisho ya siku ya Kifua Kikuu Duniani, Ummy alisema lengo la kupima makundi hayo muhimu ni kuzika kuenea kwa ugonjwa huo mapema, kwani mgonjwa mmoja ana uwezo wa kuambukiza watu 20 kwa mwaka kama hajaanza kutumia dawa kitu ambacho ni hatari.

Bweni ya wanafunzi

"Makundi hatarishi ambayo lazima wapimwe wale wanaoishi na Virusi vya Ukimwi, watoto chini ya miaka mkutano, wajawazito, wafungwa, watumiaji madawa ya kulevya, watu wanaougua saratani na kisukari lazima wapime Kifua Kikuu kwa lazima," amesema

Alisema tatizo ni kubwa nchini kwani takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa Tanzania kwa mwaka 2015 jumla ya watu 160,000 waliugua Kifua Kikuu kati ya hao watu 62,180 sawa na asilimia 39 tu ndiyo waligunduliwa na kupata matibabu.

"Hii inamaanisha katika kila watu 100,000, watu 306 wanaougua ugonjwa wa Kifua Kikuu kila mwaka nchini na kati ya hao wanaougua inakadiriwa watu 55,000 duniani wanafariki dunia kila mwaka," amesema

Amesema Mkoa wa Dar esalaam bado unaongoza kuwa na idadi kubwa yawagonjwa wa kifua kikuu ambapo waliopo ni asilimia 22, ikifuatiwa na Mwanza, Mbeya, Morogoro, Shinyanga, Arusha, Mara, Manyara, Tanga na Kilimanjaro.

"Mikoa hii pamoja na Daresalaam huchangia asilimia 63 ya wagonjwa wote waliogundulika nchini mwaka 2015," amesema

Amesema kutokana na hilo serikali imeweka mkakati kuongeza vituo vyenye mashine za kisasa za kupima kifua kikuu kutoka mashine 70 hadi kufika mashine 150 ifikapo Desemba  2017 ambapo mashine hizo kila moja ina uwezo wa kupima wagonjwa 12 kwa siku na ifikapo Juni 2018 hospitali za Wilaya na Mikoa zitakuwa na mashine hizo zenye uwezo wa kutoa majibu ndani ya saa mbili.