Jumapili , 15th Nov , 2015

Wananchi wa jimbo la Lulindi wilayani Masasi Mkoani Mtwara, leo wanapiga kura katika uchaguzi mdogo wa kumtafuta mbunge wa jimbo hilo, baada ya uchaguzi huo kuahirishwa hapo awali.

Mkurugenzi wa Uchaguzi kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi - NEC, Dkt Ramadhani Kailima.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Uchaguzi kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi Dkt Ramadhani Kailima, imesema kuwa uchaguzi huo unafanyika kufuatia makosa yaliyofanyika awali katika karatasi za kupigia kura na kupelekea uchaguzi huo kuahirishwa.

Dkt Kailima amesema Tume inasisitiza mambo muhimu mojawapo ikiwa ni pamoja na vyama vyote vya siasa vinavyoshiriki katika uchaguzi huo kuhakikisha vinaweka mawakala wake katika vituo vyote vya kupigia kura na kujumlisha kura. Mawakala hao watatakiwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa.

Aidha, mara baada ya kupiga kura na kwa kuzingatia maadili ya uchaguzi ya 2015 yaliyokubaliwa na vyama vyote vya siasa na kuridhiwa na mahakama, wapiga kura wanatakiwa kuondoka vituoni na kuendelea na shughuli zao. Vituoni vyama vya siasa vimeweka mawakala wake ambao watalinda maslahi ya vyama husika na wagombea wao.