Alhamisi , 17th Aug , 2017

Baada ya mamlaka ya chakula na dawa kanda ya kati kufunga machinjio ya manispaa ya Singida, wakazi wa manispaa ya Singida wapo hatarini kupatwa na magonjwa yatokananyo na kula nyama kufuatia baadhi ya wauza nyama kuchinja Ng'ombe bila kupimwa.

Akiteketeza kwa moto kilo themanini na nne (84) za nyama ya Ng'ombe ambazo zilikutwa zikiuzwa katika mazingira machafu huku zikiwa zimehifadhiwa chini, Mkaguzi wa chakula kutoka TFDA kanda ya kati Bwana Aberl Deule, amesema wamefikia uamuzi wa kuteketeza nyama hiyo kwa sababu licha ya machinjio kufungwa baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakichinja ng'ombe vichochoroni na kuhatarisha maisha ya walaji.

Pamoja na madai hayo, wachinjaji wanyama wa manispaa ya Singida wametupia lawama kwa mkurugenzi wa manispaa ya Singida kuacha kufanyia matengenezo na usababisha machinjio kufungwa mara kwa mara, huku wao wakiwa wamekopa fedha katika sekta za benki.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa manispaa ya Singida Bwana Deusi Luziga amekiri kuwa machinjio hayapo katika hali nzuri, ila manispaa imeanza kufanya ukarabati wa machinjio hayo na wameshatenga eneo la kujenga chinjio jingine jipya kulingana na kuongezeka kwa watu.