Ijumaa , 19th Mei , 2017

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan amewaagiza Makatibu Mahsusi nchini kufanya kazi kwa kuzingatia maadili na waache tabia ya kutoa siri za ofisi zao kwani kufanya hivyo ni kosa kisheria.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan ametoa kauli hiyo wakati anafungua mkutano wa Tano wa Chama cha Makatibu Mahsusi Tanzania mkoani Dodoma ambapo amesema uadilifu na uaminifu ni njia pekee ya kuaminiwa na viongozi wao hivyo ni muhimu kwa makatibu mahsusi nchini kufanya kazi kwa bidii na ubunifu mkubwa katika maeneo yao ya kazi.

Makamu wa Rais pia amewahimiza makatibu mahsusi kufanya tathmini ya utendaji wao wa kazi na wawe tayari katika kujifunza mbinu mpya za utendaji zinazoendana na mabadiliko ya teknolojia.

“Sote tunafahamu kuwa dunia imekuwa ni kijiji kutokana na utandawazi unaoletwa na mifumo ya teknolojia hivyo kutokana na mabadiliko haya hamna budi nanyi kubadilika na kwenda na wakati ili msiangaliwe kwa mtazamo hasi wa kuwa wapiga cha tu” -Mh. Samia.

Kuhusu uanzishwaji wa Shahada ya Uhazili, Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amewahakikishia makatibu mahsusi kuwa Serikali imekubali kuanzisha shahada hiyo ambapo masomo yake yataanza mwezi wa Tisa mwaka huu kwenye Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania katika mikoa ya Dar es Salaam na Tabora.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amewahimiza makatibu mahsusi kuchangamkia fursa hiyo kwa ajili ya kujiendeleza kielimu kwa kuzingatia kuwa elimu haina mwisho.