Jumatatu , 13th Nov , 2017

Serikali imelionya baraza la madiwani la Manispaa ya Kigoma Ujiji kuacha mara moja kushiriki kwenye Mpango wa Kimataifa wa uendeshaji wa shughuli za serikali kwa uwazi (OGP), ambao serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imejitoa.

Onyo hilo limetolewa leo bungeni na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Mh. Goerge Mkuchika wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kigoma Mjini Mh. Zitto Kabwe lilitoka kujua kauli ya serikali kutokana na ushiriki wa Manispaa hiyo kwenye mpango huo.

“Serikali inazo taarifa kuwa Manispaa ya Kigoma Ujiji mpaka sasa inawasiliana na OGP na OGP wamemwandikia barua Waziri wa mambo ya Nje  kwamba wana nia ya kuendelea kushirkiana na nyie, sasa nataka niionye Manispaa ya Kigoma Ujiji waache mara moja kuwasiliana na OGP”.

Aidha Waziri ameitaka Manispaa hiyo kutekeleza maamuzi ya serikali na endapo itaendelea basi serikali itachukua hatua kali ambazo ni kuvunja baraza la madiwani na kuweka Tume ya Manispaa. 

Waziri pia ameeleza kuwa taratibu za OGP zipo wazi kuwa nchi ikijitoa moja kwa moja ushiriki wa wanachama wengine kutoka ndani ya nchi husika unakuwa umefika kikomo hivyo Manispaa hiyo inavunja kanuni za nchi.

Tanzania imejitoa kwenye Mpango wa Kimataifa wa uendeshaji wa shughuli za serikali kwa uwazi (OGP), ambao imedumu kama mwanacham kwa miaka minne tangu ilipojiunga Septemba 21 mwaka 2011.