Jumatano , 23rd Aug , 2017

Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari, Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi amewataka wamiliki wa magazeti na majarida mbalimbali kufanya hima kuenda kujisali upya kuanzia leo kwani wasipofanya hivyo watashindwa kuendelea kuchapisha

Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari, Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi.

Dkt. Abbasi amebainisha hayo kwenye mkutano wake na waandishi wa habari na kusema endapo chombo chochote kitakaidi agizo hilo mpaka kufikia Oktoba 15 mwaka huu basi litakuwa linatenda kosa la jinai.

"Kuanzia leo hadi Oktoba 15 mwaka huu magazeti yote yahakikishe yanakuja kusajiliwa upya katika mfumo wa mpya wa utoaji wa leseni kwa machapisho yote. Mfumo mpya wa utoaji leseni ni muendelezo wa azma yetu ya kuifanya tasnia ya habari kuwa taaluma",alisema Dkt. Abbasi.

Pamoja na hayo, Dkt. Abbasi aliendelea kwa kusema "baada ya Oktoba 15 mwaka huu halitaruhusiwa gazeti au jarida kuendelea kuchapisha bila ya kuwa na usajili huu mpya wa leseni".

Mbali na hilo, Dkt. Abbasi amewakumbusha wanahabari ambao wapo chini kielimu kuhakikisha kwamba katika miaka mitano waliopewa wanafikia kiwango kilicho wekwa cha taaluma kwa wanahabari hao.

"Katika taaluma ya habari kwa wanahabari tumeweka miaka 5 wajiendeleze, wale ambao wapo chini ya Diploma wakajiendeleze", alisema Dkt. Abbasi.

Kwa upande mwingine, Dkt. Abbasi amesema kwa mujibu wa sheria vyombo vyote vitasajiliwa upya bila ya kujali kama ni jarida la Wizara au gazeti la serikali.