Jumamosi , 18th Nov , 2017

Serikali imesema asilimia 28.2 ambayo ni sawa na Watanzania zaidi ya milioni 12 hawapati mahitaji ya msingi, na kwamba kiwango cha umasikini nchini bado kipo juu.

Taarifa hiyo imetolewa na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt.Philip Mpango, wakati wa uzinduzi wa zoezi la ukusanyaji wa takwimu za utafiti wa mapato na matumizi ya kaya binafsi Tanzania bara kwa mwaka 2017/18, na kusema kwamba ni dhahiri kiwango cha umasikini kwa wananchi bado kipo juu.

Zoezi la ukusanyaji wa takwimu za utafiti wa mapato na matumizi ya kaya binafsi litafanyika katika mikoa yote ya Tanzania bara, na kutarajiwa kufikiwa kaya 10,460, huku ikielezwa kwamba kukamilika kwa zoezi hilo kutawezesha serikali kutathmini hatua zilizofikiwa katika mpango wa pili wa maendeleo ya taifa, na utekelezaji wa malengo endelevu.

Ukusanywaji wa takwimu na utafiti huo unafanywa na wadadisi 620 walioandaliwa, ambapo mkurugenzi mkuu ofisi ya taifa ya takwimu Dk. Albina Chuwa, amewataka kutoa taarifa za ukweli, vinginevyo watakaodanganya watawajibishwa kwa mujibu wa sheria ya takwimu ya mwaka 2015.

Tazama video hapa chini Waziri Mpango akielezea hilo.