Jumanne , 6th Dec , 2022

Jeshi la Polisi mkoani Arusha limesema litaendelea na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto kwa kuhakikisha wanaibua na kuwachukulia hatua watu wote wanaojihusisha na vitendo hivyo.

Makamu Mwenyekiti wa Mtandao wa Polisi wanawake (TPF NET), mkoani humo Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Edith Swebe

Hayo yamesemwa na Makamu Mwenyekiti wa Mtandao wa Polisi wanawake (TPF NET), mkoani humo Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Edith Swebe, wakati akiongea na wananchi wa jamii ya kifugaji eneo la Namanga wilayani Longido katika maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili.

SSP Swebe amesema ni wakati sasa wa jamii kuwaibua na kuwafichua watu wachache wanaofanya vitendo hivyo vya ukatili katika jamii ambapo Jeshi la Polisi litaendelea kufanya doria pamoja na kutoa elimu kuanzia ngazi ya familia, mtaa, Kata na hata wilaya ili kuhakikisha matukio ya ukatili yanaisha kabisa.

Naye Kaimu Katibu Tawala wa wilaya ya Longido kwa niaba ya Mkuu wa wilaya Boniphace Lugola, amewataka wananchi, viongozi wa vitongoji, vijiji na watendaji wa ngazi zote kila mmoja kwa nafasi yake kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kufuatilia na kuwafichua wahalifu wote wanaojihusisha na matukio ya ukatili katika jamii wanazoishi.