Jumamosi , 26th Sep , 2020

Kamati ya amani nchini inayoongozwa na Mwenyekiti wake na Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa, imepiga marufuku makanisa na misikiti, kutumika kumfanyia kampeni mgombea yoyote wa chama cha siasa kwa kuwa kufanya hivyo ni kuwanyima haki waumini wake.

Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhadi Mussa Salum.

Wametoa agizo hilo leo Septemba 26, 2020, jijini Dar es salaam, wakati wakizungumza na wandishi wa habari ambapo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Sheikh Alhadi Mussa Salum, amesema kwa kufanya hivyo inawezekana ikawa chanzo cha kuvuruga amani ya nchi.

 

"Muacheni mtu akamchague kiongozi anayemtaka na sio wewe kiongozi wa dini fulani unatumia nyumba za ibada kama ni jukwaa la kisiasa"amesema mwenyekiti wa kamati hiyo Shekh Alhad Musa Salum.

Kushoto ni Mjumbe wa kamati ya amani nchini Sylvester Gamanywa, katikati ni Mwenyekiti wa kamati hiyo Sheikh Alhad Mussa na kulia ni Makamu Mwenyekiti George Fupe.

Amesema kama kila kiongozi wa dini ataamua kufanya hivyo amani ya nchi tunaweza kuivuruga hivyo amewataka viongozi dini kushirikiana katika kupinga kutumia nyumba za ibada kunadi sera zao.