Jumatano , 22nd Nov , 2017

Msanii Nikki wa Pili ambaye ni miongoni mwa wasanii wasomi nchini, ameitwa kujiunga na chama cha ACT Wazalendo, ili kuongeza nguvu na kukijenga zaidi chama hiko.

Kiongozi wa chama cha ACT Wazalendo Zitto Zuberi Kabwe amemuandikia ujumbe kwenye ukurasa wake wa twitter kumuomba kufanya hivyo.

"Njoo ujenge Chama cha kijamaa bana acha mambo yako", ameandika Zitto Kabwe kwenye ukurasa wa Nikki wa pili.

Baada ya tweet ya Zitto Kabwe kumuomba Nikki, Nikki alimjibu kuwa chama cha kijamaa kinajengwa na watu wanyonge, bali yeye  kama mtu wa vyombo vya habari sio wa kuaminika kwani hawachelewi kuwauza.

"Chama cha kijamaa hujengwa na vugu vugu la wanyonge wenyewe, ni muwe tu na mkakati wa kuwaunganisha ki ideologia, umoja zao hizo za boda boda, machinga, wakulima, sisi watu wa media hatu kawii kuwauza sokoni kama nyanya", ameandika Nikki wa Pili.

Mpaka sasa haijulikani msanii huyo ni mfuasi wa chama gani kutokana na kuonekana kuwa mwanaharakati wa masuala ya kisiasa na uchumi, na hajawahi kuonekana kwenye jukwaa la chama chochote kufanya kampeni.