Alhamisi , 19th Oct , 2017

Aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa ACT Wazalendo Samsoni Mwigamba na wanachama wengine 10 wametangaza kujiunga na chama cha CCM baada ya kujivua uanachama wa ACT Wazalendo leo.

Taarifa za Mwigamba kujiunga na CCM zimetolewa leo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, na kusema kwamba wameamua kufanya hivyo ili kujitenga na upinzani unaokerwa na maendeleo ya nchi, na pia kuunga mkono juhudi za serikali za mapambano dhidi ya rushwa.

“CCM ya sasa ndicho chama kinachotekeleza kwa karibu itikadi, falsafa na sera za ACT Wazalendo ambazo mimi na wenzangu tulishiriki kukiasisi, nchi yetu ndio kinara wa mapambano dhidi ya rushwa sasa hivi, sera ambazo ndio misingi ya ACT Wazalendo, tumeamua kujitenga na upinzani unaokerwa na mafanikio ya nchi ili tuendelee kuwa sehemu ya mapambano katika kurejesha nchi kwenye misingi yake”, amesema Mwigamba.

Samson Mwigamba atakuwa kiongozi wa pili ACT Wazalendo kujivua uanachama wa ACT Wazalendo kwa mwaka huu baada ya Prof. Kitila Mkumbo ambaye naye alifanya hivyo wiki kadhaa zilizopita.