Jumanne , 17th Jan , 2017

Mwanamke mmoja aliyejulikana kwa jina la Anastazia Francis miaka 48 amekutwa akiwa amejinyonga hadi kufa katika mtaa Nyasaka wilaya ya Ilemela jijini Mwanza.

DCP Ahmed Msangi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza

Taarifa ya jeshi la Polisi mkoa wa Mwanza imesema kuwa mnamo tarehe 16.01.2016 majira ya saa 11:00 asubuhi, mwanamke huyo alikutwa akiwa amejinyonga hadi kufa ndani ya chumba chake kwa kutumia mtandio ambao alikuwa ameuning’iniza kwenye dirisha juu.

Inadaiwa kuwa mwanamke huyo baada ya mumewe kuondoka alimtuma mwanae mkubwa aliyemaliza kidato cha nne aende dukani na mwingine mdogo mwenye umri wa miaka 06 aende kufagia na ndipo alipopata mwanya wa kwenda kujinyonga hadi kufa.

Tukio hilo lilijulikana baada ya mtoto wake mdogo kurudi ndani chumbani kuchukua shati na kumkuta mama yake akiwa amejining’inizi ndipo aliita watu ili waje kumsaidia.

Taarifa hiyo ya jeshi la polisi imesema kuwa upelelezi unaendelea ili kufahamu chanzo cha tukio hilo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza DCP Ahmed Msangi amewaasa wananchi pindi wanapopata matatizo waombe ushauri kwa watu wengine ili kuweza kuepusha maamuzi ambayo ni hatari katika maisha yao.