Alhamisi , 20th Apr , 2017

Waziri Mkuu, Kassim Majliwa amewataka watanzania kuwa watulivu na kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi ili waweze kubaini wahusika wa matukio ya uhalifu yanayotokea nchini ikiwemo utekaji na kutoweka kwa baadhi ya watu akiwemo Ben Sanane.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa

Akijibu swali la Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Freeman Mbowe katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu bungeni Mjini Dodoma, amesema watanzania wanapaswa kuwa watulivu na kuviamini vyombo vya uchunguzi ambavyo vitakuja na majibu yatakayoonesha nini kinachoendelea nyuma ya matukio hayo.

Mh. Mbowe alitaka kauli ya serikali kuhusu matukio hayo, ikiwemo kutoweka kwa msaidizi wake Ben Sanane ambaye hadi sasa ni takriban miezi mitano imepita tangu kijana huyo atoweke, lakini akihoji sababu za serikali kutohusisha mataifa mengine yaliyoendelea katika masuala ya kiuchunguzi hususani Uingereza katika kufanya uchunguzi wa masuala ya aina hiyo.

"Kwanza nataka nikuhakikishie kwamba Taifa letu lina mahusiano na mataifa kadhaa ambayo tunashirikiana katika mambo mbalimbali ikiwemo masuala ya ulinzi ... Taifa letu lina uwezo wa ndani wa kufanya ufuatiliaji wa kutambua matukio haya ya awali, ya mtu kufariki ama kutoweka mahali baada ya familia husika kutoa taarifa, tunaweza kufanya uchunguzi na kubaini vyanzo, serikali haina kikomo cha uchunguzi kwa kutegemea na  nature ya tatizo lenyewe, uchunguzi huu utakapokamilika, taarifa itatolewa" Alisema Majaliwa

Waziri mkuu amesema “Tukitoa taarifa mapema tunaweza kuharibu upelelezi, tuviachie vyombo vetu vya dola viendelee kufuatilia kuona nani anayesababisha vitendo hivyo na dosari iko wapi na nini chanzo chake alisisitiza,”.

Kadhalika Waziri Mkuu amewasii Watanzania kuendeleza utamaduni mzuri wa watu kuheshimiana, kufuata kanuni na kuviachia vyombo vya dola kutekeleza majukumu yake. “Moja ya majukumu ya Serikali ni kuhakikisha Watanzania wanaishi kwa amani kwa kuwa na ulinzi wa uhakika kwao wenyewe na mali zao wakati wote,”.

Kwa upande mwingine, Majaliwa amemjibu Kiongozi wa Upinzani kuwa suala la kurusha matangazo mubashara ya shughuli za Bunge yalishafikiwa katika Bunge lililopita na serikali itaendelea kuboresha kila wakati namna ya urushwaji wa matangazo hayo.