Alhamisi , 17th Aug , 2017

Mapacha walioungana kuanzia kifuani hadi tumboni wamefariki dunia jana katika hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam walipokuwa wakipatiwa matibabu baada ya kuzaliwa katika hospitali ya Berege wilayani Kilosa mkoani Morogoro.

Afisa uhusiano wa hospitali ya Taifa Muhimbili, Neema Mwangomo amethibitisha kufariki kwa watoto hao ambao walikuwa wakisubiri kufanyiwa upasuaji, huku akisema kuwa uchunguzi unafanyika kubaini chanzo cha kifo cha watoto hao.

Watoto hao waliozaliwa wakiwa na uzito wa kilo nne walipewa rufaa ya kupelekwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ili kupatiwa uangalizi zaidi na waliwasili katika hospitali hiyo Juni 24 na kuwekwa katika chumba cha uangalizi maalum.

Daktari bingwa wa upasuaji wa watoto, Dkt. Zaituni Buhari Agosti 2 mwaka huu alieleza wanahabari kuwa  watoto hao walikuwa wanachangia ini na sehemu ndogo ya moyo lakini wangeweza kufanyiwa upasuaji.

Hata hivyo baadhi ya mapacha wa aina hiyo ambao hawajawahi kufanyiwa upasuaji na kufanikiwa kuishi na kuwa watu wazima ni pamoja wale wanaoishi wilayani Kilolo mkoani Iringa na wamehitimu kidato cha sita mwaka huu na kupata ufaulu mzuri wa kuendelea na elimu ya juu..