Jumamosi , 25th Mar , 2017

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imebaini makontena mengine 262 yenye mchanga wa dhahabu yaliyokuwa yamehifadhiwa katika bandari kavu ya MOFED (zamani ZAMCARGO) iliyopo Kurasini jijini Dar es salaam.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Mhandisi Deusdedit Kakoko, akiongela kubainika kwa makontena yenye mchanga wa dhahabu 262 katika bandari ya Dar es salaam leo tarehe 25 Machi, 2017 Wengine katika picha ni maafisa wa TPA na Kamanda wa Polisi Kikosi cha Bandari Ramadhani Mungi

Makontena hayo yalikuwa yakisubiri taratibu za kiforodha kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi kupitia kitengo cha makontena kinachoendeshwa na kampuni binfasi ya TICTS.

Kubainika kwa makontena hayo kumekuja siku tatu tu baada ya Rais Magufuli kutembelea bandari ya Dar es salaam na kukagua makontena 20 yenye shehena ya mchanga wa madini kutoka migodi mbalimbali iliyopo Kanda ya Ziwa.       

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Mhandisi Deusdedit Kakoko, amesema makontena hayo yaliyokuwa katika hatua za mwisho kukamilisha taratibu za kiforodha yamebainika leo tarehe 25 Machi, 2017 katika msako mkali unaoendeshwa na Mamlaka yake.

Mhandisi Kakoko amesema makontena yote hayo yalikuwa na lakiri (seals) za Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA), na yalikuwa yanashughulikiwa na kampuni ya usafirishaji wa mizigo ya Freight Forwarders Tanzania Limited iliyopo Dar es salaam.

Amesema jumla ya makontena 256 yalikuwa katika bandari kavu ya MOFED, wakati makontena mengine sita yalikuwa tayari yameshaingizwa bandarini tayari kwa kusafirishwa.

Ametoa wito kwa makampuni yote ya madini yenye shehena za mchanga yajitokeze yenyewe na kuonesha mizigo yao popote ilipo nchini kabla haijabainika katika msako kabambe unaondeshwa na vyombo vya ulinzi na usalama katika maeneo mbalimbali nchi nzima.

Orodha ya makontena hayo yaliyobainika inaonesha yalifika bandarini hapo katika nyakati tofauti kutoka migodi ya Buzwagi na Pange Mines.

Kamanda wa Polisi Kikosi cha Bandari Bw. Ramadhani Mungi amesema bandari zote nchini ziko salama na kwamba ulinzi na usalama umeimarishwa kwa kuwekwa askari na vifaa vya kisasa vya ulinzi zikiwemo kamera.