Jumamosi , 25th Mar , 2017

Chama  cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kimewapitisha makada wake Ezekiel Wenje na Lawrence Masha kugombea nafasi za ujumbe katika Bunge la Afrika Mashariki katika uchaguzi utakaofanyika mapema mwezi ujao.

Masha (kushoto), Wenje (kulia)

Akizungmza na wanahabari jana, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho upande wa Tanzania Bara John Mnyika amesema makada hao wamepitishwa na Kamati Kuu ya chama hicho, baada ya kupitia sifa na vigezo vya makada kadhaa walioomba nafasi hizo.

Kwa mujibu wa Mnyika, CHADEMA ina nafasi mbili kati ya 9 za uwakilishi kwenye bunge hilo kutoka Tanzania, na wao wameamua kupitisha majina mawili pekee ili kurahisisha kazi wakati wa uchaguzi.

"Kulingana na uwiano wa wabunge katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CCM wana nafasi 6, CHADEMA tuna nafasi mbili, na CUF wana nafasi moja, kwahiyo tumeamua kupitisha majina mawili pekee ambayo sasa yatasubiri baraka za wabunge wa Bunge la Tanzania" Alisema manyika.

John Mnyika

Ikumbukwe kuwa makada waliopitishwa wamewahi kuwa mahasimu wakubwa wa kisiasa hasa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambapo wote wawili walikuwa wakigombea jimbo moja la Nyamagana Jijini Mwanza wakiwa vyama tofauti.

Wakati huo, Masha alikuwa CCM, na alikuwa ni Waziri wa Mambo ya Ndani huku akitaka kulitetea jimbo lake, lakini alijikuta akipata upinzani mkali kutoka kwa Wenje (CHADEMA), ambapo matokeo yalimuangusha Masha na Wenje kuwa mbunge wa jimbo hilo kwa miaka mitano kabla ya kuangushwa katika uchaguzi wa mwaka 2015 na Stanslaus Mabula (CCM)