Ijumaa , 30th Oct , 2015

Aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Mapinduzi ambaye kwa sasa ndiye Rais mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli leo anatarajiwa kukabidhiwa hati ya ushindi kutoka tume ya taifa ya Uchaguzi(NEC).

Rais Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Joseph Pombe Magufuli akiwa na Makamu wake wa Rais Mama Samia Hassan Suluhu

Hapo jana tume hiyo imemtangaza Dk. John Pombe Magufuli kuwa mshindi wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kushinda katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu ambapo ushindi huo utaenda sambamba na mgombea wake mwenza mama Samia Suluhu Hassan.

Akitangaza matokeo hayo leo jijini Dar es Salaam, mwenyekiti tume hiyo jaji Mstaafu Damian Lubuva amesema Dk. John Pombe Magufuli amepata kura 8, 882, 635 sawa na asilimia 58.46, akifuatiwa na mgombea wa Chadema Edward Ngoyai Lowassa aliyepata kura 6,072,848 sawa na asilimia 39.97.

Jaji mstaafu Lubuva ameeleza kuwa katika uchaguzi mkuu jumla ya wapiga kura 23,121, 440 walijiandikisha kupiga kura, waliopiga kura ni 15,585,639 sawa na asilimia 67.31, kura halali zilizopigwa ni 15, 193,861 sawa na asilimia 97.49,.