Jumatatu , 21st Aug , 2017

Kesi iliyokuwa ikimkabiri Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Mhe. Godbless Lema imehairishwa hadi Septemba 20 mwaka huu ambapo itasikilizwa tena.

Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Mhe. Godbless Lema.

Hayo yamebainishwa mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Arusha, Devota Msofe, Mwanasheria wa serikali Agnes Hiera ambapo alieleza kuwa kesi ya Lema ilikuwa inatakiwa kusomewa maelezo ya awali ya mashtaka yanayomkabiri lakini kwa bahati mbaya majalada yake yameitwa kwa Mkurugenzi wa mashtaka nchini.

Baada ya maelezo hayo, Wakili wa utetezi Sheck Mfinaga ameiomba Mahakama leo ndiyo iwe kuweka aihirisho la mwisho kwa kesi zinazomkabiri Lema kwani zimekuwa zikiahirishwa mara kwa mara.

Awali, Mei 29 mwaka huu, Hakimu Mkazi Desdery Kamugisha ambaye alikuwa akisikiliza kesi hizo alijitoa kuendelea kusikiliza kesi namba 441/2016, ambapo Lema anadaiwa kutoa matamshi yenye chuki na kuibua nia ovu kwa jamii. 

Mhe. Godbless Lema alikaa Mahabusu ya gereza kuu la Kisongo kwa zaidi ya miezi minne, kutokana na kukosa dhamana katika kesi iliyokuwa inamkabiri na kuja kuachiwa kwa dhamana Marchi 3 mwaka huu na Mahakama Kuu Kanda ya Arusha.