Ijumaa , 17th Nov , 2017

Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema kupitia CHADEMA, ameweka wazi matatizo anayoyapata kama mbunge wa wananchi wake anaowatumikia, na kusema kwamba kama viongozi wao wanaumia zaidi wanapoona hawawaelewi wanachokifaya.

Lema ameyasema hayo kwenye mkutano wa hadhara akifanya kampeni kwa ajili ya chaguzi ndogo ndogo za udiwani katika kata ya Muriet mkoani Arusha, na kueleza kwamba wao kama wabunge wao wanajitoa muhanga kuwatetea wananchi wao, lakini huwa wanaumia zaidi pale wananchi hao kuonekana hawajali wala hawaoni jitihada zao.

Mimi ni mbunge ambaye nimekaa hospitali kumuuguza mbunge mwenzangu ambaye amepigwa risasi. Tundu Lissu amepigwa risasi kwa sababu ya kutetea uhuru wenu, tukiona hamuelewi mnatuumiza kuliko hao wanaotupiga, kama kuna kuna mateso tunapata kama viongozi wenu ni wakati nyie ambao tunawapigania hamtuelewi, tunaumia kuliko maelezo”, amesema Godbless Lema.

Godbless Lema ameendelea kwa kusema kwamba yeye binafsi anakumbana na changamoto nyingi kwani tangu apate wadhifa huo hajawahi kupata raha, kutokana na misuko suko anayoipata kutoka kwa jeshi la polisi na kudhalilishwa.

Toka nimekuwa mbunge wenu sijawahi kupata raha katika uongozi wangu, mimi ni mbunge ambaye nimepigwa sana, nimedhalilishwa sana na polisi, ni mbunge ambaye nyumbani kwangu polisi wamesachi mpaka nguo za ndani za mke wangu, kunidhalilisha na kutisha, nimekwenda jela miezi minne na siku 12, nimetekwa ili kuuawa, nimefukuzwa bungeni, kesi nilizonazo ni nyingi, nina kesi mbili dhidi ya Rais na siogopi, na haya yote kwa ajili yenu nyinyi”, amesema Godbless Lema.

Godbless Lema amekuwa mbunge ambaye mara kwa mara anakabiliana na jeshi la polisi kwa makosa mbali mbali anayotuhumiwa, ambapo mpaka sasa bado ana kesi zinazomkabili mahakamani.