Jumamosi , 15th Jul , 2017

Naibu Waziri wa Afya Dk. Hamisi Kigwangalla ametoa maagizo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Tunduru kuboresha huduma za afya wilayani hapo hasa kituo cha afya  Mkasale ambacho kinatoa huduma mbovu pamoja na uchakavu wa majengo.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Hamisi Kigwangalla akizungumza katika mkutano huo wa wazi kwa wananchi wa Halmashauri ya Tunduru, Mkoani Ruvuma

Akiwa katika ziara  ya kikazi ya ukaguzi wa utekelezajiwa agizo la uboreshaji wa vituo vya afya katika kila Kata nchini lilitolewa Desemba 2016, Dk. Kigwangalla  akikagua kituo hicho cha Mkasale amesema  uchakavu wa majengo  hali inayo hatarisha usalama na afya za watumishi na wagonjwa wanaohudumiwa hapo na kuutaka uongozi wa Halmashauri hiyo kushughulikia suala ndani ya miezi mitatu ikiwemo Mkandarasi wa Maji kuhakikisha anaingiza mifumo ya maji ndani ya kituo hicho.

Aidha Dk Kigwangalla amewaambia wananchi wa Tunduru  Serikali inaendelea na uboreshaji wa huduma za afya na kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma zenye ubora na kwa wakati na lengo likiwa ni kupunguza kwa asilimia kubwa changamoto zinazoikabili wilaya hiyo ikiwa ni pamoja na kupunguza vifo vya kinamama wajawazito na watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, kukamilisha maboma yote ya vituo vya afya, zahanati na hospitali ambazo hazijakamilika, na kuhakikisha kuwa vifaa tiba na dawa zinapatikana za kutosha.

"Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa kuhakikisha kuwa dawa zinakuwepo za kutosha katika hospitali na vituo vya afya na katika mwaka wa fedha 2017/2018  serikali imetenga bajeti ya kutosha kuhakikisha kuwa vifaa tiba vinakuwepo katika vituo vya afya na hospitali zote nchini. Samabamba na hayo serikali inahakikisha kuwa huduma za mama na mtoto zinatolewa bure kwenye hospitali za umma zote nchi ili kupunguza vifo vya wamama wajawazito na watoto walio chini ya umri wa miaka mitano", alisema

Pamoja na hay Dk Kigwangalla aliuagiza uongozi wa kijiji cha mkasale na mkotamo kutengeza barabara ya kuelekea katika kituo cha afya mkasale kutoka na barabara hivyo kuwa chafu sana hali inayoweza kuleta madhara kwa watumiaji hasa kwa wadudu kama nyoka.

"Nakuagiza mwenyekiti wa kijiji mara baada ya kumaliza kikao hapa upange ratiba na wananchi wako namna bora ya kuweza kutengeza barabara inayokwenda katika kituo cha afya mkasale na pia mupange ratiba ya kufanya ausafi katika kituo kwani kazi ya usafi ni ya wananchi," - alisema Dk kigwangalla.

Naibu waziri wizara ya Afya, Jinsia, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto Dk. Hamisi Kigwangalla akilakiwa na wananchi  wa Kijiji cha Mkasale wilayani Tunduru, Mkoani Ruvuma wakati wa ziara yake hiyo

Aidha, katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma zilizo bora uongozi wa wilaya umeagizwa kufanya kuhakikisha vituo vyote vya afya vilivyopo wilayani Tunduru, vinajenga  vyumba vya upasuaji katika vituo vyote vya afya, kukarabati maabara zote, na kuhakikisha kunakuwepo na mfumo wa maji safi  wenye uhakika katika vituo vyote vya afya, kufanya matengenezo kwa vifaa vilivopata hitilafu ili kuboresha huduma.