Jumatatu , 28th Sep , 2020

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam imeahirisha kesi ya mchekeshaji Idriss Sultan na mwenzake ya kushindwa kusajili laini ya simu iliyokuwa ikitumiwa na mtu mwingine.

Akieleza mbele ya Hakimu Mkazi mfawidhi, Rashid Chaungu, wakili wa serikali Kija Elias, amesema shauri hilo lilikuja kwa ajili ya kuanza kusikiliza ushahidi ambapo upande wa utetezi uliowakilishwa na Wakili Jebra Kambole, umeomba tarehe nyingine.

 Awali upande wa utetezi uliomba muda wa kufanya kikao kwa ajili ya kukiri kosa ''bargaining'' ambapo wamedai kuwa hawakupata muda wa kufanya kikao hicho.

Aidha Hakimu Chaungu, ameutaka upande wa utetezi kuja na majibu kamili ili kama watashindwa kufanya kikao hicho basi mahakama hiyo ianze kusikiliza ushahidi na kesi hiyo imeahirishwa hadi Oktoba 29,mwaka huu.

Idris anakabiliwa na shitaka la kushindwa kusajili laini ya simu iliyokuwa ikitumiwa na mtu mwingine ambapo mshtakiwa mwingine katika kesi hiyo ni mfanyabiashara Innocent Maiga anayekabiliwa na kosa la kushindwa kutoa taarifa ya mabadiliko ya umiliki wa laini ya simu hiyo.