Jumatatu , 25th Jan , 2021

Waziri wa TAMISEMI, Selemani Jafo, amesema kuwa kutokana na stendi mpya ya mabasi ya Mbezi Luis kuwa na hadhi ya kimataifa, anapendekeza ipewe jina la Rais Dkt. Magufuli, kama seemu ya shukrani na kuthamini jitihada alizofanya na kwamba atamuomba ili aridhie ombi hilo.

Waziri wa TAMISEMI, Selemani Jafo

Kauli hiyo ameitoa hii leo Januari 25, 2021, alipotembelea kujionea hali ya uenzi wa stendi hiyo, ambapo pia ameuagiza uongozi wa mkoa wa Dar es Salaam, kuhakikisha stendi hiyo inaanza kutumika muda wowote kuanzia sasa.

Mbali na hayo Waziri Jafo, pia amemuelekeza mkandarasi anayejenga eneo la maegesho ya magari madogo, kuhakikisha anakamilisha kazi ndani ya wiki mbili kuanzia leo huku akitaka taa zifungwe ndani ya wiki moja kuanzia leo, huku akiupongeza uongozi wa mkoa kwa usimamizi mzuri uliosaidia stendi hiyo kukamilika kwa ubora unaotakiwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa jiji la Dar es Salaam Spora Liana, amesema kazi zinazoendelea kwa sasa ni ufungaji wa viyoyozi, lifti, ufungaji wa taa na vifaa vya matangazo, uunganishwaji wa maji kwenye vyoo na miundombinu mingine ambayo nayo ipo hatua ya mwisho kukamilika.