Alhamisi , 23rd Mar , 2017

Balozi wa Hungary hapa nchini mwenye makazi yake Nairobi, Kenya Mhe. Lazaro Eduard Mathe amemhakikishia Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli kuwa nchi yake ipo tayari kushirikiana na Tanzania katika kuendeleza sekta ya viwanda

Rais Magufuli akipokea hati za utambulisho kutoka kwa Balozi wa Hungary Mhe. Lazaro Eduard Mathe

Pia Balozi huyo amemuhakikishia kwamba wawekezaji kutoka Hungary wameanza kufanya mchakato wa kujenga kiwanda cha kuunda mabasi ya abiria.

Mhe. Lazaro Eduard Mathe amesema hayo leo Ikulu Jijini Dar es Salaam, wakati akizungumza na Mhe. Rais Magufuli muda mfupi baada ya kukabidhi hati zake za utambulisho akiwa ni miongoni mwa Mabalozi sita waliokabidhi hati hizo.

Pamoja na nia ya kujenga kiwanda cha kuunda mabasi ya abiria, Mhe. Lazaro Eduard Mathe amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa juhudi kubwa anazofanya kujenga uchumi wa Tanzania na ameahidi kuwa Hungary itakuza na kuimarisha ushirikiano wake na Tanzania kwa kuleta teknolojia katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda na kilimo pamoja na kuwahimiza wawekezaji kuja kuwekeza nchini Tanzania.