Alhamisi , 23rd Nov , 2017

Mbunge wa Kigoma Mjini Zitto Zuberi Kabwe, amesema kitendo cha watu kujazana kufuata matibabu kwenye meli ya wachina iliyopo bandarini, inadhihirisha ni namna gani wananchi wanashindwa kumudu gaharama za matibabu, na iwe somo kwa Taifa

Zitto Kabwe ameyasema hayo kwa kuandika ujumbe kwenye ukurasa wakewa facebook na kusema kwamba taifa lenye hali kama hii haliwezi kupiga hatua kimaendeleo, hata kama wakijenga miundombinu ya kisasa, na kuitaka serikali kuweka misingi imara kwenye jamii yake.

"Nimepita kituo cha reli ya kati Dar na kuona msururu wa watu. Nimeambiwa wanakwenda kwenye meli ya madaktari wa wachina. Hii ni ishara kuwa watu wetu wanaumwa na hawana uwezo wa kuhudumia afya zao. Taifa lenye hali hii haliwezi kamwe kusonga mbele hata lijenge fly overs kila kona. Maendeleo ni watu, hili liwe somo. Tujenge Hifadhi ya Jamii ya Taifa ili tuwe na Taifa lenye afya bora na Uchumi shirikishi", ameandika Zitto Kabwe.

Hivi karibuni meli kutoka china yenye madktari bingwa imetia nanga kwenye bandari ya Dar es salaam, na kutoa huduma ya matibabu kwa wakazi wa jiji hilo bila gharama zozote.