Jumapili , 24th Jan , 2021

Taifa Stars imefufua matumaini ya kufuzu hatua ya robo fainali ya michuano ya timu za taifa kwa wachezaji wa ndani (CHAN) inayoendelea nchini Cameroon, baada ya kushinda mchezo wake wa pili Kundi D kwa goli 1-0 dhidi ya Namibia.

Wachezaji wa Taifa Stars wakishangilia goli

Goli pekee la Taifa Stars katika mchezo huo lilifungwa na winga wa Yanga Farid Musa dakika ya 65, hivyo kuifanya Tanzania kufikisha pointi 3 ikiwa katika nafasi ya 3 nyuma ya vinara Zambia wenye pointi 4 na Guinea wanaoshika nafasi ya pili wakiwa pia na pointi 4 wakizidiwa magoli na Zambia.

Kwa jinsi msimamo wa Kundi D ulivyo, Tanzania sasa inahitaji kupata pointi 3 dhidi ya Guinea kwenye mchezo wa mwisho wa kundi hilo utakaopigwa Jumatano Januari 27, 2021.

Endapo Taifa Stars itapata ushindi huo moja kwa moja itakuwa imefuzu robo fainali hata kama Zambia itashinda au kufungwa na Namibia kwenye mchezo mwingine wa mwisho wa kundi D.

Michezo yote miwili ya kufunga Kundi D itapigwa muda mmoja ambao ni saa 4:00 usiku kwa saa za Afrika Mashariki.