Jumapili , 18th Apr , 2021

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Aboubakar Kunenge amezitaka DAWASA na TANESCO kufanya kazi kwa ushirikiano na mkandarasi JASCO Building and Civil Contractor anayejenga Barabara ya Makongo kwa kuondoa miundombinu ya maji na umeme iliyopita kwenye mradi.

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Aboubakar Kunenge

Kunenge ameyasema hayo alipofanya ziara ya kukagua miradi minne ya maendeleo Jijini humo ambapo amemtaka mkandarasi huyo kuhakikisha ujenzi inakamilika kabla ya Mwezi Oktoba. 
 
''Taasisi za DAWASA na TANESCO fanyeni kazi kwa ushirikiano na mkandarasi ili asipate kisingizio chochote cha kuchelewesha kazi hii inayotakiwa kukamilika Oktoba,'' amesema.

Aidha Mkuu huyo wa mkoa amesema barabara hiyo yenye urefu wa Km 4.5 ni moja ya barabara muhimu katika kutatua changamoto ya foleni kwenye barabara ya Bagamoyo, ambapo mradi huo umegharimu zaidi ya Bilioni 8.2.