Jumamosi , 17th Apr , 2021

Jeshi la Polisi mkoani Kagera linamshikilia Joachim Rwegasira mwenye umri wa miaka 45 mkazi wa kitongoji cha Rushonga kata Buganguzi wilayani Muleba kwa tuhuma za kuwaua mke na mtoto wake mdogo mwenye umri wa mwaka mmoja, kwa kuwakata na kitu chenye ncha kali.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Maketi Msangi

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Maketi Msangi amesema kuwa tukio hilo limetokea Aprili 16 mwaka huu saa tisa Alasiri, na kuwataja waliouawa kuwa ni Rosemary Joachim mwenye umri wa miaka 35 na mtoto wake Joiness Joachim mwenye umri wa mwaka mmoja.

Msangi amesema kuwa chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa kimapenzi na kwamba baba huyo amekuwa akimlalamikia mke wake kuwa ana mahusiano ya kimapenzi na jirani yao na kwamba hata mtoto huyo alimzaa na jirani, ambapo baada ya kutekeleza mauaji hayo mtuhumiwa huyo alijaribu kujiua bila mafanikio.

"Mtuhumiwa alijikata kwa kitu chenye ncha kali sehemu za tumboni katika kitovu na shingini akilenga kujidhuru lakini hakufanikiwa na  alikamatwa akiwa hai", amesema.

Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda huyo, mtuhumiwa huyo amelazwa katika hospitali teule ya wilaya ya Muleba iitwayo Rubya, kwa matibabu na hali yake sio nzuri.