Jumatatu , 27th Mar , 2017

Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Magufuli, amelitaka jeshi la polisi nchini kuhakikisha linamwachia huru msanii wa muziki wa kizazi kipya, Emmanuel Elibariki maarufu Nay wa Mitego, aliyekamatwa mjini Morogoro jana.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mjini Dodoma, Waziri wa Habari, Utamaduni na  Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe, amesema Rais Magufuli amesema wimbo wa 'wapo' ulioimbwa na msanii huyo ni mzuri hivyo kutakiwa upigwe.

Mwakyembe amesema Rais amesema 'biti' zilizomo katika wimbo huo ni nzuri na anafurahishwa nazo hata maneno yake yanafikisha ujumbe kwa jamii.

"Nimechukua hatua kama waziri mwenye dhamana kuagiza polisi wamuachie yule kijana na kuwaomba BASATA waache kumuhoji huyo kijana, nashauri BASATA wamshauri aje Dodoma ili tushauriane mambo ya kuongeza, wimbo utakuwa mzuri kweli, mimi mwenyewe nimeisikiliza ile biti, naungana na Rais, kwa kweli ile biti kali" Amesema Mwakyembe

Agizo hilo limetoka saa chache baada ya Baraza la Sanaa Tanzania la Taifa (BASATA) kutangaza kuufungia kwa madai ya kukiuka baadhi ya kanuni katika maudhui yake.

Msikilize hapa Waziri Mwakyembe akiongea na waandishi wa habari leo mjini Dodoma

 

Sauti: Dkt. Harrison Mwakyembe