Jumamosi , 12th Jun , 2021

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limesema kuwa linamshikilia kijana mmoja aliyefahamika kwa majina ya Shedrak Kapanga (34), amabye alikuwa ni msaidizi wa kazi za ndani kwa tuhuma za kumuua bosi wake na watoto wake wawili kwa madai ya kwamba amekuwa akimgombeza mara kwa mara.

Emmy Mutaboyerwa (katikati) na wanaye Daniela na Damita Mutaboyerwa.

Taarifa hiyo imetolewa leo Juni 12, 2021, na Kamanda wa kanda hiyo Muliro Jumanne, wakati akizungumza na Radio One na kueleza kuwa tukio hilo limetokea Juni 9, 2021, maeneo ya Masaki Dar es Salaam, na mtuhumiwa amekamatwa jana Juni 11, 2021, maeneo ya Magomeni akiwa kwenye harakati za kutoroka.

Waliofariki ni Emmy Mutaboyerwa ambaye ni Mama na mabinti zake wawili Daniela na Damita Mutaboyerwa.

Aidha taarifa imeongeza kuwa mara baada ya mtuhumiwa huyo kukamatwa wakati akijiandaa kutoroka alikutwa na simu za marehemu, Television na king'amuzi cha DSTV na remote.

Kamanda Muliro ameeleza kuwa upelelezi wa tukio hilo umebaini kwamba, mtuhumiwa alimpiga kila mmoja na kitu kizito na kuwasababishia kuvuja damu nyingi na baada ya kuwauwa aliwafungia ndani na kisha yeye kutoroka.